Monday, 14 July 2014

Baadhi ya wahitimu nchini humaliza ngazi ya mbalimbali za elimu na kutunikiwa lakini hawana uelewa wa kutosha wa kile walichokisomea pia hukosa wa juu ya mamboyanayoendelea kwenye mazingira husika.by Bi Riziki Abraham ambaye ni msemaji wa Sekretarieti ya Ajira nchini


NI ukweli ulio wazi kwamba kumekuwako na ongezeko la idadi kubwa ya vijana wanao hitimu elimu ya vyuo vikuu nchini  ambao wamekuwa wakilalamika kukosa nafasi za ajira katika makampuni na mashirika mbalimbali.
 Suala la  vijana hao kukosa ajira limekuwa likiongezeka kadri siku zinavyosonga mbele na hivyo kuwa si  geni tena miongoni mwetu na wala halina kificho kwa sababu tumekuwa tukiwashuhudia kila siku wengi wao wakirandaranda mitaani bila kazi maalumu.
 Hali hiyo hupelekea wengi wao kuingiwa na tamaa na kujikuta wakifanya vitendo viovu ambavyo havikubaliki katika jamii ikiwamo uvunjaji wa sheria,utapeli na kujihusisha na biashara haramu, ili wajipatie kipato cha kuendesha maisha yao.
  Hata hivyo mfumo mbovu wa elimu bado ni kilio cha watanzania wengi kutokana na kuzalisha wahitimu tegemezi wasio weza kupambana katika  soko la ajira  za ndani na za kimataifa jambo ambalo hupelekea ajira nyingi kuchukuliwa na wageni japo kuwa vyuo vyetu hapa nchini vimekuwa vikizalisha wahitimu wengi kila mwaka.
Ili kutatua tatizo hilo Serikali kupitia Wizara ya Kazi na Ajira, imekuwa ikibuni mipango mbalimbali ambapo hivi karibuni ulizinduliwa mfumo maalum wa kielektroniki wa taarifa za ajira.
 Licha ya kuzinduliwa kwa mfumo huo lakini bado kuna umuhimu wa kujitathimini upya katika suala la mfumo mzima wa elimu kwa kuwepo ongezeko la wastani wa 48% wanafunzi wanao jiunga na elimu ya juu nchini lakini bado wengi humaliza wakiwa na elimu ya nadhalia kuliko vitendo katika fani walizosomea na kuonekana hawana uwezo na ubora katika soko la ajira ndani na nje ya nchi .
Katika kulitambua hilo, serikali kupitia Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, imeamua kuweka mkazo katika suala hilo ili kuhakikisha kuwa utumishi wa umma unakuwa na watumishi wenye weledi  wa hali ya juu kupitia mchakato wa ajira
Bi. Riziki Abraham ambaye ni msemaji wa sekretarieti hiyo, anasema lengo la Serikali ni kuhakikisha inapata  waombaji wenye sifa kitaaluma, uwezo na ujuzi ili kuufanya utumishi wa umma unaendeshwa na watu wenye weledi na maadili mema katika kuiwezesha serikali kutimiza malengo yake kwa ufanisi.
“Kwa kuwa nchi nyingi duniani na hususani kwenye utumishi wa umma zimeweza kuendelea kwa kasi kubwa kutokana na kuwa na Rasilimali Watu wenye kukidhi viwango na weledi wa hali ya juu, Rasilimali Watu wenye sifa ni nguzo muhimu katika utendaji kazi ulio bora na wenye kufikia malengo katika sehemu yeyote iwe za huduma au uzalishaji,”anasema.
Anasema upatikanaji wa Rasilimali watu bora inategemea sana na uwepo wa wahitimu bora kutoka katika vyuo na taasisi za  elimu ya juu zilizopo katika nchi husika.
“Baadhi ya wahitimu  nchini humaliza ngazi mbalimbali za elimu na kutunukiwa vyeti lakini hawana uelewa wa kutosha wa kile walichokisomea pia hukosa ufahamu wa juu ya  mambo yanayoendelea kwenye mazingira husika, ”anafafanua.
Anasema wengi wa wahitimu hao hutarajia wawe na uwezo wa kujiajiri au kuajiriwa pindi wamalizapo masomo yao katika sekta binafsi na zile za umma kutokana na weledi wa kuendana na soko la ajira katika karne hii ya sayansi na teknolojia.
Bi. Abrahamu anasema kwa miaka minne sasa tangu  Sekretarieti ya Ajira ipewe jukumu hilo, imekuwa ikikabiliana na changamoto mbalimbali ikiwemo ubora wa wahitimu wanaowasilisha maombi ya kazi serikalini kuanzia waombaji wenye elimu ya ngazi ya Sekondari, Astashahada, Stashahada, Stashahada ya juu, Shahada, Shahada ya Uzamili pamoja Shahada ya Uzamivu.
“Sekretarieti ya Ajira katika tathimini yetu tumebaini mapungufu mbalimbali yatokanayo na ubora wa wahitimu wa ngazi mbalimbali za elimu ya juu ambao huomba ajira kupitia chombo hiki na hata wale walioko kazini.
“Hata hivyo tofauti ya mapungufu yao hutofautiana kutoka ngazi moja na nyingine, uwezo wa kitaaluma na ufahamu, kuamini vyeti peke yake vinaweza kuwapa kazi pasipokuwa uelewa mpana wa kile walicho ombea kazi, kutotilia maanani sifa au vigezo na masharti ya tangazo husika na kutokujiamini pia.
kukosa  uzoefu kwa kazi inayohitaji uzoefu, uwezo mdogo wa mawasiliano ikiwemo matumizi ya lugha sahihi, uwezo mdogo wa kutumia nyenzo za utendaji kazi hususani vifaa vya kieletroniki, kutojiandaa vya kutosha, kukosa mbinu za usaili na kutozingatia muda,” anasema.
Anasema changamoto nyingine ni kutokujitambua kwa baaadhi ya wahitimu ambapo wengine husoma kwa kufuata mkumbo na hivyo kukosa sifa halali za kitaaluma, kutokujua namna ya kuandika barua za maombi ya kazi, namna ya kuandika wasifu wao (CV), kutokuwa na maandalizi sahihi pamoja na kughushi baadhi ya sifa kwa lengo la kujipatia ajira.
“Wahitimu wanaoomba kazi wakitokea kazini baadhi yao wameonyesha udhaifu wa kutokuwa na uwezo wa kukabiliana na changamoto hivyo kuona bora atafute kazi nyingine, kutokupitisha barua kwa wajiri, kukosa uelewa mpana unaoendana na uzoefu wake kazini ili kuweza kuonyesha tofauti yake na waajiri wapya, kukimbilia Serikalini ilikupata fursa ya kusomeshwa lakini si kwa lengo la kwenda kuongeza tija kiutendaji,”anasema.
Bi. Abraham anasema hali hii inadhihirisha kwamba wapo waombaji kazi ambao wanasoma ili kufaulu au kuhitimu na sio kuelewa kwa ufasaha fani wanazosomea ili kuweza kuleta utaalamu wao katika nyanja mbalimbali za maendeleo.
“Hali hii hupelekea kuchangia kushindwa kufikia hatua ya kuitwa kwenye usaili kutokana na kukosa baadhi ya vigezo na wengine kufikia hatua ya usaili na kushindwa kufaulu usaili husika kutokana na kutokujiandaa ipasavyo,” anasema
Dkt. Benson Bana ni Muhazili  wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), katika kitengo cha rasilimali watu (human resouce), yeye anaonekana kwenda tofauti na tathimini hiyo kwa kudai haijaangalia kwa undani changamoto wanazosema wahitimu hao.
Anasema  vyuo vikuu na taasisi nyingine za elimu ya juu hutoa mafunzo kwa jumla kama maarifa yatakayo msaidia muhitimu, lakini mafunzo ya kazi  huyapata akiwa kazini.
“Wahitimu wetu ni bora tafauti na nchi zingine ila ni juhudi za muajiri kuhakikisha  anaandaa mazingira mazuri na mafunzo ya kazi kwa vitendo kwa wale anaotaka kuwaajiri, kiuwalisia uwezi kutarajia mwanafunzi anapomaliza miaka minne  akawa weza kumudu  mazingira kwa haraka.
 “Kazi ya vyuo ni kutoa maarifa  na kuwaanda wahitimu lakini elimu ya kazi anatakiwa kuipata akiwa kazini,”anasema Bana.
Anasema muhitimu hawezi kufanya kazi tofauti na vigezo vinavyotakiwa  na mwajili wake, ukiona mpaka anaajiliwa anakuwa katimiza vigezo vyote na kwamba zipo taaluma zinazo tegemeana kulingana muhitimu  alisomea kitu gani.
Anasema nchi yetu bado inatatizo la mbinu za kutumia katika  usaili kwa kuwa mbinu nyingi zinazo tumiwa ni zakizamani na hazitoshi kuweza kujua uwezo wa mtu kwa kuwa hata hao wanaosaili hawana uwezo na mbinu zao zimepitwa na wakati.
“Mimi kama mtaalamu wa rasilimali  watu hapa nchini,bado tunahitaji kujipanga kutafuta mbinu nzuri zaidi ya moja ambazo zitatusaidia kupata wahitimu na watendaji kazi wanao hitajika,kwa kuwa  mbinu zinazotumiwa zimepitwa na wakati katika kufanya usaili na kutokana na mbinu hizo hatuwezi kupata watendaji wazuri kwa kuwa hata hao wanao fanya usaili hawana uwezo unaotakiwa.
 “Nimesha wahi kufanya kazi na sekretarieti ya ajira hapa nchini, kwa hiyo najuwa uzahifu wao, usaili mwingi unafanyika kwa kutumia njia moja tu ambayo ni  maswali, na utakuta hao wanao fanya usaili hawajapewa elimu ya kusaili inapelekea hata maswali wanayo uliza kuwa tofauti na malengo ya kazi vilevile kingereza sio sehemu ya kupata mtendaji mwadilifu  kwa maana mtu anaweza kujua kingereza  bado akawa sio mtendaji mzuri,” anasema Bana.
Anasema dunia ya leo inahitaji mabadiliko, cheti ni kigezo cha kugundua kiwango cha elimu ya muhusika na ni lazima mwajili ajue anatafuta mfanyakazi wa aina gani na awe tayari kumuendeleza kwa kumpa mafunzo ya kazi ili mwajiriwa apate uzoefu na katika kutekeleza hilo, ni lazima mwajili alifanye ipasavyo  asikwepe wajibu wake.
Akichangia hoja hiyo, mwanafunzi wa mwaka wa tatu, anayechukua shahada ya elimu katika chuo kikuu cha St john, Nuru Masera, anasema baadhi ya vyuo na taasisi za elimu ya juu, wahadhili wake wengi hawana viwango vinavyo hitajika na serikali.
“Baadhi ya vyuo wanafundishwa na wahadhili ambao hawana viwango labda kwa kuwa wengi wamemaliza degree, kinyume na agizo la serikali,pia vigezo vya ajira kwa waajiri  wengi  uwa vikubwa tofauti na hali alisi  ambayo wahitimu wengi wanavyo, ” anasema Masera.
Masera anasema licha ya uzembe wa mwanafunzi mwenyewe katika kuakikisha anajisomea na kutambua wajibuwake pia suala la semina ambazo zimekuwa zikiendeshwa katika vyuo nayo inaonekana kualibu latiba ya mwanafunzi.
“Utakuta kipindi kinaendelea uku mwanafunzi yupo kwenye semina labda anategemea amwombe mwenzie amuelekeze baada ya kumaliza na kwa kuwa ratiba ya kipindi cha darasani na semina zimekuwa sambamba anajikuta hana jinsi,”anafafanua.
Anasema kutokana na baadhi ya taaluma hazipewi kipaumbele na serikali, wanafunzi hujikuta wanabadili taaluma  wanayosomea au kazi kutokana na maslahi au mazingira ya kazi husika yalivyo.
“Wahitimu wengi hujikuta wanafanya kazi kutokana na maslahi na mazingira duni kwa baadhi ya ajira , ndio yanayopelekea wanafunzi kubadili taaluma wanayosomea na mwajili hawezi kukuajili kama hautakuwa na vigezo anavyo vitaka kwa vile taaluma nyingi hutegemeana,”anafafanua Masera.

No comments:

Post a Comment