 |
| Rais Putin akimpokea Rais Al-Sisi, Sochi |
Rais wa Urusi, Vladmir Putin amekutana na mwenzake wa Misri, Abdel
Fattah al-Sisi, ambapo pamoja na mambo mengine wamejadiliana kuhusu
masuala ya ushirikiano mkubwa wa kijeshi, teknolojia na biashara huria.
Rais Putin ameahidi kuharakisha hatua ya kupeleka silaha za mabilioni ya
dola nchini Misri, na ameikaribisha nchi hiyo katika biashara huria.
Viongozi hao wawili wameimarisha uhusiano wao tangu Putin alipomuunga
mkono Al-Sisi wakati wa ziara yake mjini Moscow mwezi Februari, kipindi
alichokuwa anagombea urais wa Misri.
Putin amesema mwezi Machi mwaka huu nchi hizo mbili zilisaini itifaki
zinazolingana na kwamba wanapeleka silaha nchini Misri na wako tayari
kutanua ushirikiano huo.
Aidha, Al-Sisi amemshukuru Rais Putin kwa kuwa kiongozi wa kwanza nje ya
mataifa ya Kiarabu, kumualika tangu alipoapishwa kuliongoza taifa lake.
Alisema watu wote wa Misri wanaifatilia ziara yake na wanategemea
kuwepo kwa ushirikiano wa hali ya juu kati ya mataifa hayo mawili.
Rais Al-Sisi akisalimiana na Rais Putin
Urusi imechukua jukumu la kupeleka silaha Misri, baada ya Marekani
kusitisha kupeleka silaha kutokana na ukandamizaji uliofanywa na Al-Sisi
baada ya kuiondoa madarakani serikali ya zamani ya Kiislamu, mwaka
uliopita.
Baada ya mkutano wa viongozi hao wawili, gazeti la kila siku la biashara
la Urusi la Vedemosti limeripoti kuwa Urusi na Misri zimesaini mpango
unaokaribia Euro bilioni 2.2 wa makombora na ndege za kivita,
utakaofadhiliwa na Saudi Arabia na Umoja wa Falme za Kiarabu.
Misri inapendelea zaidi mifumo ya ulinzi wa anga
Mkuu wa kituo cha utafiti wa biashara ya silaha duniani mjini Moscow,
Igor Korotchenko, amesema Misri inapendelea zaidi mifumo ya ulinzi wa
anga. Amesema anadhani kusainiwa kwa mikataba halisi ni suala la muda tu
na kwamba makubaliano katika ngazi ya kisiasa tayari yameshafikiwa.
Ama kwa upande mwingine, Rais Putin ameikaribisha Misri kuanzisha ukanda
wa biashara huru kati ya Misri na umoja wa ushuru na forodha wa Urusi,
Belarus na Kazakhstan. Urusi imesema itaongeza kiwango cha kupeleka
ngano nchini Misri na kuingiza bidhaa nyingine za kilimo kutoka Misri.
Viongozi wa Urusi na Misri wakizuru kituo cha michezo ya kuteleza kwenye theluji, Sochi
Urusi inaangalia vyanzo vipya vya usambazaji wa bidhaa, baada
ya wiki iliyopita kupiga marufuku chakula kutoka Marekani, Umoja wa
Ulaya, Australia, Canada na Norway, ikiwa ni katika kujibu hatua ya
vikwazo vilivyowekwa dhidi yake kutokana na mzozo wa Ukraine.
Akizungumza baada ya kukutana na Rais Al-Sisi, Putin amesema tayari
Misri imeongeza usambazaji wa bidhaa za kilimo kwenye soko la Urusi kwa
asilimia 30 na iko tayari kuongeza asilimia nyingine 30 katika siku
zijazo.
Waziri wa Kilimo wa Urusi, Nikolai Fyodorov, amewaambia waandishi wa
habari mjini Sochi kuwa kuongezeka kwa chakula kama vile viazi,
vitunguu, vitunguu saumu na machungwa kutoka Misri, kutasaidia kufidia
nusu ya upungufu wa bidhaa hizo uliosababishwa na hatua ya kupiga
marufuku.